Tuesday, December 19, 2017

UVCCM YAKAMILISHA UHAKIKI WA KURA ZILIZOPIGWA 10/12/2017 DODOMA.

Umoja  wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umefanya uhakiki wa kura zilizopigwa katika uchaguzi wa jumuiya hiyo ngazi ya Taifa na kubaini kuwa viongozi wote waliochaguliwa wamechaguliwa kihalali.

Aidha umetoa onyo kwa wale wote  wanaojivika joho la kuwa wasemaji wa jumuiya kuacha mara moja kwa kuwa mamlaka za usemaji zipo kwa mujibu wa kanuni na katiba.

Kaimu katibu wa UVCCM Taifa Shaka Hamdu Shaka akizungumza na waandishi wa habari leo mjini Dodoma amesema kama jumuiya walipokea agizo kutoka kwa Mwenyekiti wa CCM Taifa Rais John  Pombe  Magufuli  kufanya uhakiki upya ili kujiridhisha iwapo haki imetendeka na kila mmoja amepata anachostahili zoezi ambalo limekamilika na tayari wameshakabidhi taarifa ya uhakiki huo katika mamlaka za chama.

Amesema zoezi hilo walilifanya kwa kushirikiana na vyombo vya dola ambavyo vina mamlaka ya kusimamia heshima na nidhamu na kusisitiza kuwa UVCCM imesimamia uchaguzi huo kwa haki na usawa na  umakini mkubwa na kwa  kutanguliza maslahi ya Taifa mbele bila ya kufanya ubabaishaji na hila vile wana dhamira ya  dhati kumuunga mkono Rais Magufuli.

" Tunaposema tunamuunga mkono  Rais Magufuli sio  kwa maneno ni  kwa vitendo katika hili Rais Magufuli ni muumini wa kweli wa kusimamia haki na usawa  hapendi wala hayuko tayari kuona mambo ya hovyo yakifanywa ili kumuumiza mwanachama au mtu yeyote   tunamshukuru sana na kumpongeza Mwenyekiti Magufuli" alisema Shaka

Hata hivyo Shaka  amekiri uwepo wa matatizo madogo sana  wakati wa kuweka kura matatizo ambayo kwa namna moja ama nyingine hayakuwaondolea ushindi  waliotangazwa ambao wameshinda kihalali kabisa

Amesisitiza na kukuendelea kuwaomba Vijana  wote kuendelea na umoja, utulivu  na mshikamano na kuungana pamoja na mwenyekiti mpya Kheir James katika kufikia dhamira ya dhati aliyonayo  kufanyia mabadiliko makubwa umoja  huo kimfumo,  kiutawala na kiutendaji.

Katika uchaguzi wa UVCCM ngazi ya Taifa uliofanyika jumapili tarehe 10 Disemba mwaka huu  ndugu Kheir James alichaguliwa kwa kura 319 kati ya kura 583 pamoja na wajumbe NEC  wajumbe wa  baraza na wajumbe wa kuwakilisha katika jumuiya za UWT na Wazazi.

No comments:

Post a Comment