Saturday, December 15, 2018

MHE KEMILEMBE: ‘MAENDELEO HAYANA CHAMA’

Tutaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo hata maeneo ya wapinzani kwa sababu shughuli za maendeleo hazina chama wala hazihitaji ubaguzi sisi wote lengo letu ni moja kujiletea maendeleo.

Kauli hiyo imetolewa leo na Mbunge wa Viti maalumu wa mkoa wa Mwanza Mhe Kemilembe Lwota wakati akikabidhi vifaa vya kutolea huduma za afya katika kituo cha afya Buzuruga kilichopo kata ya Buzuruga manispaa ya Ilemela vikiwemo vitanda 10, magodoro 10 na mashuka 20 vyenye thamani ya Jumla  ya Shilingi Milioni Nane Laki Moja na elfu Tisini na Tisa ambapo amesema kuwa Serikali ya chama cha mapinduzi  chini ya Rais Mhe Dkt John Magufuli itaendelea kuthamini afya za waTanzania  kwa kutekeleza miradi mikubwa ya afya ili kuhakikisha afya za wananchi wake zinakuwa imara na nzuri bila kujali tofauti zao za kiitikadi za vyama vya siasa ama nyenginezo

‘… Maendeleo hayana chama, maendeleo hayabagui ukiwa ccm, ukiwa chadema ni lazima utatumia huduma zinazotolewa kituo hapa …’ Alisema

Aidha Mhe Kemilembe amempongeza Mbunge wa Jimbo la Ilemela Mhe Dkt Angeline Mabula sambamba na kuwaomba wananchi wa jimbo hilo kuendelea kumuunga mkono  kwa jitihada kubwa anazozifanya katika kuhakikisha anawatumikia wananchi wake na kuwaletea maendeleo

Akimkaribisha Mbunge huyo wa Viti maalumu, Mbunge wa Jimbo la Ilemela Mhe Dkt Angeline Mabula  mbali na kushukuru, amempongeza Mhe Kemilembe kwa kuunga mkono jitihada za Mhe Rais katika kuimarisha sekta hiyo ya afya huku akiwaasa wananchi wa Jimbo hilo kuendelea kuchangia huduma za afya pamoja na kuanzisha miradi ya maendeleo inayotekelezwa kwa utaratibu wa utatu kwa maana ya kuhusisha nguvu za wananchi, nguvu za mbunge na nguvu za serikali kupitia halmashauri ya manispaa ya Ilemela.

Akisoma risala kwa mgeni rasmi, mtaalamu wa huduma za afya ya uzazi na mtoto kwa manispaa ya Ilemela  Bi Nyabwire Lukumai mbali na kutaja changamoto zinazokabili kituo hicho cha afya, ametaja zahanati zitakazonufaika na msaada huo wa vifaa vya kutolea huduma za afya vilivyotolewa kuwa ni zahanati ya Nyamhongolo, zahanati ya Ilemela, Zahanati ya Nyakato, Zahanati ya Kabusungu na Zahanati ya Nyamwilolelwa.

Akihitimisha Diwani wa kata ya Buzuruga, Mhe Richard Machemba ameshukuru kwa msaada huo huku akiwaomba wananchi kuendelea kumpa ushirikiano mbunge wa jimbo hilo na mbunge huyo wa viti maalumu kwa namna wanavyojitoa katika kutekeleza shughuli za kimaendeleo hasa katika kata yake bila kujali tofauti za kiitikadi za kichama.


Makabidhiano hayo pia yalihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa CCM ngazi ya wilaya na mkoa wakiongozwa na katibu wa CCM wilaya ya Ilemela Achen Maulid na katibu wa UWT mkoa wa Mwanza.

' Ilemela ni yetu, tushirikiane kuijenga'

Imetolewa na
Ofisi ya mbunge
Jimbo la Ilemela
14.12.2018










No comments:

Post a Comment