Sunday, December 16, 2018

TATIZO LA UMEME ILEMELA KUWA HISTORIA.

Tatizo la ukosefu wa umeme katika mitaa ya manispaa ya Ilemela yenye sura ya kijiji kuwa historia ifikapo Januari, 2019.

Kauli hiyo imetolewa leo na meneja wa shirika la umeme nchini (TANESCO) kwa kanda ya Ilemela mkoa wa Mwanza Mhandisi Ezekiel Simon Mashola akijibu maswali ya wananchi wa Kata ya Shibula juu ya ukosefu wa Umeme wa uhakika wakati wa ziara ya Mbunge wa Jimbo la Ilemela ambae pia ni Naibu Waziri wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe Dkt Angeline Mabula iliyofanyika katika mtaa wa Semba ili kusikiliza changamoto, kero na ushauri kutoka kwa wananchi hao juu ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kimaendeleo jimboni humo ambapo amewahakikishia kuwa kabla ya Januari 31, 2018 maeneo yote ya jimbo hilo yatakuwa na umeme wa uhakika baada ya kupatikana kwa vifaa vitakavyotumika kukamilisha mradi wa umeme vijijini (REA) kwa awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza  mara baada ya kusimama kwa mradi huo kufuatia kukosekana kwa vifaa

‘… Changamoto iliyokuwa inamkabili mkandarasi ilikuwa ni vifaa ndio mana mkaona kama mradi umefifia hivi, Lakini hivi karibuni tulikuwa na kikao na mkandarasi wa REA, Mkurugenzi wa REA na baadae Waziri wa nishati pale Dodoma, Transifoma zishafika, nguzo zipo, mita zimefika tunachosubiria ni utekelezaji tu …’ Alisema

Aidha Mhandisi Ezekiele ameongeza kuwa jumla ya mitaa 7 ya Buganda, Semba, Lwashi, Iponyabugali, Igalagala, Kabusungu na Lutongo itanufaika na huduma hiyo kwa 100% huku mitaa itakayosalia ikipangwa katika awamu ya tatu mzunguko wa pili unaotaraji kuanza hivi karibuni.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Ilemela Mhe Dkt Angeline Mabula mbali na kumshukuru Rais Mhe Dkt John Magufuli kwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuwasisitiza vijana kutumia fursa za upatikanaji wa mikopo na elimu ya ujasiriamali ili kijikwamua kiuchumi, amesema kuwa  mpaka sasa 89%  ya ahadi zake alizozitoa wakati akiomba kura kwa wananchi amekwisha zitekeleza ikiwemo kuboresha miundombinu ya Elimu ambapo vyumba vya madarasa vimejengwa kupitia mradi wa ufatuaji matofali chini ya taasisi ya The Angeline Foundation, kuboresha mazingira katika vituo vya afya na zahanati ambapo zahanati mpya zimezidi kujengwa ikiwemo ile ya Buganda, Lukobe na Nyamhongolo sambamba na kuzipandisha hadhi zile za zamani kuwa vituo vya afya huku jengo la dharula la hospitali ya wilaya likikamilika kwa zaidi ya 90%, kuanzisha mashindano mbalimbali ya michezo ambapo mashindano ya Angeline Ilemela Jimbo Cup yamekuwa yakifanyika kwa lengo la kuibua vipaji vipya na kuviendeleza vile vya zamani, kusogeza huduma ya maji kwa wananchi ambapo mbali na shirika la maji safi na maji taka MWAUWASA kutekeleza miradi mbalimbali mbunge kwa kushirikiana na wadau wameweza kujenga visima katika maeneo tofauti tofauti kurahisisha upatikanaji wa huduma hiyo muhimu.

Nae Diwani wa kata hiyo, Mhe Dede Swila kwa niaba ya wananchi wa kata hiyo amemshukuru mbunge huyo kwa kazi kubwa anayoifanya katika kuwaletea maendeleo huku akiahidi ushirikiano, Sanjari na kuwaomba wazee wa kata hiyo kuacha mambo ya kishirikina ili watumishi wa umma waliopo katika kata yao waweze kufanya shughuli zao kwa weredi.

‘ Ilemela ni yetu, tushirikiane kuijenga’

Imetolewa na
Ofisi ya mbunge
Jimbo la Ilemela
15.12.2018.











No comments:

Post a Comment