Monday, December 17, 2018

DKT ANGELINE MABULA: TUENDELEE KUMUUNGA MKONO JPM

Wananchi wa Jimbo la Ilemela wametakiwa kuendelea kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt John Joseph Pombe Magufuli kwa utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo anayoifanya.

Rai hiyo imetolewa na Mbunge wa Jimbo la Ilemela Mhe Dkt Angeline Mabula wakati akizungumza na wananchi wa kata ya Bugogwa katika viwanja vya Kabangaja ikiwa ni muendelezo wa ziara yake ya kusikiliza kero za wananchi, changamoto na ushauri zinazowakabili ili kujiletea maendeleo, Mhe Dkt Angeline Mabula amewataka wananchi hao kumshukuru na kuendelea kumuunga mkono Rais Magufuli kwa mageuzi makubwa anayoendelea kuyafanya ili kufikia uchumi wa kati kupitia sera ya viwanda ambapo miradi mikubwa ya kimaendeleo imeendelea kutekelezwa ikiwemo ununuzi wa ndege za kisasa, ujenzi wa reli ya kisasa(SGR), uboreshaji wa sekta ya afya na kuongeza bajeti ya sekta hiyo, ujenzi wa mradi wa ufuaji wa umeme(Striggers Gauge), upanuzi wa viwanja vya ndege na ujenzi wa miundombinu ya barabara na madaraja pamoja na kutoa elimu bure kwa shule za msingi na sekondari hadi kidato cha nne.

‘… Tuna Rais anaejali watu wake hasa wale wanyonge, amefuta shuru na tozo zote zilizokuwa kero, ameamua kutoa vitambulisho kwa wafanyabiashara wadogo wenye mtaji wa chini ya milioni 4 ambao hawapo kwenye mfumo wa mamlaka ya ukusanyaji kodi (TRA) ili waweze kukua kiuchumi, Mungu atupe nini ndugu zangu zaidi ya kumuombea na kuendelea kumuunga mkono …’ Alisema

Aidha Mhe Dkt Mabula amekemea kitendo cha kutwaa ardhi za wananchi bila kulipa fidia kama taratibu na sheria za ardhi na mipango miji zitakuwa zimefuatwa huku akiwaasa wananchi hao kuhakikisha wanalipa gharama za urasimishaji makazi na kuhakikisha wanachukua hati ili kuongeza thamani ya maeneo yao sanjari na kuwaasa wafanya biashara wakubwa kuacha kudanganya ili waweze kunufaika na vitambulisho vya wafanyabiashara wadogo vilivyotolewa na Mhe Rais.

Kwa upande wake afisa ardhi wa manispaa ya Ilemela, Ndugu Shukran Kyando amesema kuwa mpaka itakapofika Januari, 2019 wananchi wa mitaa ya Nyafula, Lugeye na Sangabuye waliokuwa katika mradi wa upimaji wa ardhi na makazi kwa awamu ya kwanza watakuwa wamelipwa fidia huku akiwaasa kuwa wavumilivu na kuendelea kutoa ushirikiano kwa wataalamu ili kumaliza salama zoezi hilo.

Akifunga mkutano huo Mwenyekiti wa Mtaa wa Kabangaja, Ndugu Sebastian Lukona amemuomba Mbunge wa Jimbo hilo kufikisha salamu wa wananchi wa mtaa wake kwa Rais Mhe Dkt John Magufuli na kuongeza kuwa wananchi wake wanaunga mkono kazi kubwa ya kuleta maendeleo anayoifanya na kuahidi kuendelea kumuunga mkono.

Ziara ya mbunge Mhe Dkt Angeline Mabula pia ilihudhuriwa na wataalamu wa manispaa ya Ilemela, shirika la maji MWAUWASA, wakala wa barabara TARURA, shirika la umeme TANESCO, na Madiwani wa kata za Sangabuye, Bugogwa na Shibula.
‘ Ilemela ni yetu, tushirikiane kuijenga’

Imetolewa na
Ofisi ya Mbunge
Jimbo la Ilemela
17.12.2018.







No comments:

Post a Comment