Monday, December 24, 2018

MBUNGE WA ILEMELA AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA KITUO CHA AFYA LUMALA

Mbunge wa jimbo la Ilemela Mheshimiwa Daktari Angeline Mabula ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa kituo cha afya Lumala kilichopo kata ya Ilemela na kugharimu zaidi ya shilingi 40,490,000 kikiwa katika hatua ya kukamilika kwa Boma.

Akizungumza na wananchi wa mtaa wa Lumala Daktari Mabula amewapongeza wananchi hao kwa utayari wao wa kuunga mkono jitihada za Serikali katika kusogeza huduma muhimu kwa jamii kwa kukubali kuchangia kiasi cha shilingi 6,990,000 kilichotumika kwaajili ya kukamilisha msingi wa kituo hicho kabla ya yeye kutoa matofali yote ya ujenzi wa boma la kituo hicho


‘… Niwapongeze sana wana Lumala ni mitaa michache sana ambayo wananchi wake wako teyari kujitokeza na kuchangia ujenzi wa miundombinu muhimu kama shule na zahanati, Wengi wanangojea Serikali ifanye na ndio maana mliponifata kunishirikisha sikusita kwa sababu niliona nguvu yenu …’ Alisema

Aidha Mheshimiwa Mabula amemuomba mkurugenzi wa manispaa ya Ilemela kuhakikisha anamalizia hatua iliyobaki ya kupaua jengo hilo  kama wanavyoshirikiana katika kutekeleza miradi mingine ya maendeleo, Kwa sera ya utatu kwa maana ya wananchi kuchangia gharama za msingi, mbunge kujenga boma na manispaa kupaua.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Ilemela Mheshimiwa Wilbard Kilenzi amemshukuru mbunge huyo kwa kuunga mkono jitihada za wananchi wa kata yake huku akimuomba kuendelea kutoa msukumo kwa ngazi  husika ili kituo hicho kiweze kufunguliwa kwa wakati uliokusudiwa.

Mara baada ya uwekaji jiwe la msingi mheshimiwa mbunge ameendelea na ziara yake ya kusikiliza kero za wananchi, changamoto, ushauri na kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo mradi wa ujenzi wa viwanja vya michezo ya mpira wa miguu, mpira wa mikono, na mpira wa pete vinavyojengwa eneo la Sabasaba katika kata hiyo akiambatana na viongozi wa shirika la maji safi na mazingira MWAUWASA, shirika la umeme TANESCO, wakala wa barabara za vijijini na mjini TARURA, wakuu wa idara za manispaa ya Ilemela, viongozi wa vyama vya kisiasa na dini.

' Ilemela ni yetu, tushirikiane kuijenga'

Imetolewa na
Ofisi ya mbunge
Jimbo la Ilemela
24.12.2018










No comments:

Post a Comment