Saturday, May 19, 2018

DKT ANGELINE MABULA: JUKUMU LA KUBORESHA MIUNDOMBINU YA SHULE SI LA SERIKALI PEKE YAKE

Mbunge wa Jimbo la Ilemela ambae pia ni Naibu Waziri wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe Dkt Angeline Mabula amewaasa wazazi kushiriki katika kuboresha miundombinu ya shule ili kutengeneza mazingira rafiki ya kufundishia na kujifunzia badala ya kuiachia Serikali peke yake
Kauli hiyo imetolewa leo na Katibu wa Ofisi ya Mbunge  wa Jimbo la Ilemela, Ndugu Michael Goyele alipomwakilisha mbunge huyo katika ufunguzi wa  mafunzo ya kujitambua na kushiriki katika kutatua changamoto zinazowakabili  wasichana yanayotolewa  na Taasisi isiyo ya Serikali ya Tanzania Youth Alliance For Development and Cooperation TYADCO iliyopo jijini Mwanza katika shule ya sekondari Buswelu ambapo mbali na kuelezea hatua mbalimbali zilizochukuliwa katika kuhakikisha sekta ya Elimu inaimarika ndani ya Jimbo la Ilemela ikiwemo ujenzi wa mabweni ya wasichana kwa shule ya sekondari Buswelu, ugawaji wa vitabu kwa baadhi ya shule za Jimbo hilo, ukarabati wa shule kongwe za Bwiru wasichana na wavulana, ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa shule za msingi na sekondari kupitia mradi wa ufatuaji tofali unaoendeshwa na taasisi ya The Angeline Foundation pia amewaasa wazazi kuhakikishia wanaunga mkono jitihada za serikali katika kuweka mazingira rafiki ya utoaji wa elimu nchini badala ya kuacha jukumu hilo kwa serikali peke yake  jambo linalochangia kudumaa kwa elimu
‘…  Jukumu la kuboresha miundombinu ya shule si la Serikali peke yake, Ingawa tumekuwa tukiona hatua mbalimbali zinazochukuliwa na serikali kama utoaji wa elimu bure na  ugawaji wa vitabu mashuleni lakini na sisi wazazi tunaowajibu katika kuboresha mazingira ya utoaji wa elimu kwa watoto wetu…’ Alisema
Aidha amewaasa wanafunzi kuzingatia masomo na kujiepusha na mazingira hatarishi yanayokwamisha ufikiaji wa ndoto zao kwa kujiingiza katika vitendo viovu  kama kubeba mimba kabla ya wakati na utumiaji wa madawa ya kulevya huku akiahidi kompyuta kwa shule ya Buswelu pamoja na kuwasomesha wanafunzi watakaofanya vizuri katika mtihani wao wa kidato cha nne mwaka huu kwa kupata daraja la kwanza
Akimkaribisha mgeni rasmi mkurugenzi wa taasisi ya TYADCO Ndugu Aloyce Masana mbali na kumshukuru Mbunge wa Jimbo hilo kwa kukubali kushiriki katika ufunguzi huo,  amewataka wanafunzi waliohudhuria mafunzo hayo kuitumia elimu waliyoipata kwa maslahi mapana ya taifa sanjari na kuzitaka taasisi binafsi kuendelea kuiunga mkono serikali katika kutatua changamoto za kijamii
Akisoma risala kwa mgeni rasmi,  mwanafunzi Sabrina Mohamedi Musa amezitaja changamoto mbalimbali zinazoikabili shule yao ikiwa ni pamoja na idadi ndogo ya walimu wa masomo ya Sayansi, vifaa vya kujifunzia, maji na mabweni huku akiomba kupatikana ufumbuzi wa haraka ili waweze kufanya vizuri katika masomo yao
Mafunzo hayo pia yalihusisha taasisi mbalimbali ikiwemo Benki ya NMB, Benki ya CRDB, Wataalamu kutoka hospitali ya mkoa Mwanza SekeuToure na Wataalamu wa halmashauri ya manispaa ya Ilemela
‘ Ilemela ni yetu, tushirikiane kuijenga’

Imetolewa na
Ofisi ya mbunge
Jimbo la Ilemela
19.05.2018






No comments:

Post a Comment