Wednesday, June 27, 2018

ILEMELA YAZINDUA MAJARIBIO YA MRADI WA UDHIBITI MAJANGA KIELEKTRONIKI

Halmashauri ya manispaa ya Ilemela imezindua majaribio ya mradi wa udhibiti majanga kielektroniki utakaotekelezwa kuanzia June 01, 2018 na kugharimu zaidi ya dola milioni tano za kimarekani kwa kushirikiana na jiji rafiki la Daegu la nchi ya Korea ya kusini, taasisi ya Egis labs, shirika la teknolojia (NIPA) kwa ufadhili wa shirika la maendeleo la nchi ya Korea kusini la KOICA

Akizungumza katika uzinduzi huo mstahiki meya wa manispaa ya Ilemela Mheshimiwa Renatus Mulunga amesema kuwa uzinduzi wa mradi huo umekuja wakati sahihi kwa manispaa yake kwani imekuwa ikikabiliwa na majanga makubwa ya mafuriko na moto kwa baadhi ya maeneo yake huku akiomba kurithishwa taaluma hiyo kwa wataalamu wake ili mradi huo uweze kuwa endelevu

‘… Tunawashukuru sana wenzetu kutoka nchini Korea, tunaamini mradi huu umekuja wakati sahihi kwani watu wetu wamekuwa wakikabiliwa na majanga makubwa ya mafuriko kipindi cha mvua na moto hivyo kuzinduliwa kwa mradi huu hivi leo kutaleta tija na chachu katika kudhibiti majanga haya …’ Alisema

Kwa upande wake kiongozi wa ugeni huo kutoka nchini Korea ya kusini  ndugu Kim Dae Wuk mbali na kufafanua juu ya umuhimu wa mradi huo  kwa jamii katika udhibiti wa majanga na utekelezwaji wake amewataka wataalam wa manispaa ya Ilemela na viongozi wake kutoa ushirikiano ili kufanikisha mradi na kuwa endelevu

Akihitimisha uzinduzi huo mkurugenzi wa manispaa ya Ilemela John Wanga mbali kuahidi ushirikiano na kushukuru kwa kuanzishwa mradi huo ameongeza kuwa hayo ni matunda ya jitihada za mbunge wa jimbo la Ilemela Mheshimiwa Daktari Angeline Mabula kama muasisi wa ushirikiano na urafiki wa jiji la Daegu na manispaa ya Ilemela katika shughuli mbalimbali za kijamii zenye lengo la kuwaletea wananchi unafuu wa maisha na maendeleo

Uzinduzi wa mradi huo ulihudhuriwa na  wataalam kutoka manispaa ya Ilemela, vyombo vya ulinzi na usalama vya wilaya hiyo na viongozi mbalimbali

' Ilemela ni yetu, tushirikiane kuijenga'







No comments:

Post a Comment