Saturday, September 15, 2018

KIRUMBA YATINGA FAINALI MASHINDANO YA ANGELINE JIMBO CUP 2018.

Mashindano ya Angeline Jimbo Cup 2018 yamezidi kutimua vumbi ambapo kwa siku ya leo yamezikutanisha Timu ya Kata ya Kirumba na Timu ya Kata ya Nyakato ikiwa ni hatua ya nusu fainali, mechi iliyochezwa katika uwanja wa Sabasaba kata ya Ilemela.
Katika mchezo huo Timu ya Kata ya Kirumba imefanikiwa kufuzu kuingia hatua ya fainali ya mashindano hayo mara baada ya kuinyuka Timu ya Kata ya Nyakato goli moja kwa sifuri, Goli lililofungwa na mchezaji Baraka David mwenye jezi nambari sita dakika ya 66 ya kipindi cha pili.
Akizungumza mara baada ya kuisha kwa mchezo huo, Diwani wa Kata ya Kirumba Mhe Alex Ngusa ameipongeza timu yake kwa ushindi ilioupata huku akiwaasa wananchi wa kata hiyo na mashabiki wote kuhakikisha wanaendelea kuunga mkono timu yao ili iweze kuchukua kombe hilo
‘.. Tumefika nusu fainali tunaelekea hatua ya fainali sasa na ni umoja, ushirikiano na upendo wa wana Kirumba ndo umetufikisha hapa, Kwa hiyo naomba nitoe wito kwa wana Kirumba waendelee kuiunga mkono timu yao …’ Alisema
Kwa upande wake msemaji wa Timu ya Kata ya Nyakato ambae pia ni Katibu wa uhamasishaji na chipukizi wa UVCCM wa kata hiyo, Ndugu Edwin Simon amelalamikia Timu pinzani kwa kukiuka sheria na taratibu za mashindano inayokataza kushirikisha wachezaji wanaocheza ligi kuu na wachezaji wasiotoka maeneo husika huku akiomba kuchukuliwa hatua kwa Timu ya Kata ya Kirumba kwa kukiuka utaratibu huo.
Aidha katika mchezo huo, Mchezaji Selemani Hamisi jezi nambari Tano anaechezea Timu ya Kata ya Kirumba alipewa Kadi Nyekundu mara baada ya kumchezea rafu mshambuliaji wa Timu ya Kata ya Nyakato.
Mashindano ya Angeline Jimbo Cup 2018 yataendelea tena hapo kesho saa 2.00 asubuhi katika uwanja wa Sabasaba kata ya Ilemela kwa kuzikutanisha timu ya kata ya Ibungilo na timu ya kata ya Shibula na fainali yake kufanyika siku ya jumatatu Septemba 17, 2018 katika uwanja wa CCM Kirumba mgeni rasmi akiwa Naibu Waziri wa Sera, Bunge Kazi ,Ajira, Vijana na Walemavu Mhe Antony Mavunde.
‘ Ilemela ni yetu, tushirikiane kuijenga’

Imetolewa na
Ofisi ya mbunge
Jimbo la Ilemela
14.09.2018.










No comments:

Post a Comment